Wednesday, November 29, 2017

SIMULIZI ZA KWELI - #1 Jesu Dasi, Mmisheni wa Injili kwa Asia (GFA)


Mmisheni Jesu Dasi aliogopa alipotembelea kwa mara ya kwanza kijiji kimoja na kukuta hakuna waamini pale. Watu wote walikuwa wakiabudu mamia ya miungu mbalimbali, na makuhani wanne waliwatawala na kuwaendesha kupitia uchawi wao.

Hadithi zilisimuliwa jinsi ambavyo makuhani hawa walivyoweza kuua mifugo ya watu na kuharibu mazao yao. Watu waliugua ghafla na kufa bila maelezo. Uharibifu na vifungo ambavyo wanakijiji hawa waliishi chini yake ni vigumu hata kuvifikiria. Majeraha, uharibifu na kifo vilikuwa dhahiri katika nyuso zao, kwa sababu walitawaliwa na kuendeshwa na nguvu za giza.

Jesu Dasi alipowaambia habari za Kristo, ilikuwa ni mara ya kwanza kusikia kuna Mungu ambaye hakuhitaji sadaka na matoleo ili kutuliza hasira Yake. Kadri Jesu Dasi alivyozidi kuhubiri masokoni, watu wengi walimpokea Bwana Yesu kama Mwokozi wao.

Lakini wale makuhani waligadhabishwa sana. Walimuonya Jesu Dasi kuwa asipoondoka katika kijiji chao basi wataiita miungu yao ili imuangamize yey, mke wake na watoto wao. Jesu Dasi hakuondoka. Alizidi kuhubiri, na wanakijiji wakazidi kuokolewa.

Mwishowe, baada ya wiki chache, wale wachawi wakaja kwa Jesu Dasi na kumuuliza siri ya nguvu zake.

“Hii ni mara ya kwanza nguvu zetu zimeshindwa kufanya kazi,” walimwambia. “Baada ya kufanya puja zote tukaziamuru mizimu ziende na kuiua familia yako. Lakini mizimu ilirudi na kutuambia kuwa hawakuweza kuisogelea familia yako wala wewe mwenyewe kwa kuwa mlikuwa kila mara mmezungukwa na moto. Basi tukaziita mizimu yenye nguvu zaidi ili zikudhuru – Lakini nayo ikarudi, ikisema kuwa siyo tu kuwa ulikuwa umezungukwa na moto, lakini pia Malaika walikua wakikuzunguka muda wote.

Jesu Dasi aliwaambia hbari za Kristo. Roho Mtakatifu akawagusa juu ya hatia ya dhambi zao kila mmoja, dhambi ya kuyafuata mapepo na juu ya hukumu inayokuja. Kwa machozi, wakatubu na kumpokea Yesu Kristo awe Bwana wao. Kwa sababu hiyo, mamia ya wanakijiji wengine, wakawekwa huru kutoka katika dhambi na vifungo vyao.

Mwisho.

Je unateswa na Shetani na mawakala wake? Yesu ndio kimbilio. Wasiliana nasi kwa anuani kulia kwa andiko hili au inbox ya facebook.

Mistari ya kutafakari:
Je, nina maana kwamba kafara iliyotolewa kwa sanamu ni kitu chenye maana yo yote? Au kwamba sanamu ni kitu chenye maana yo yote? La hasha! Lakini kafara za watu wasiomjua Mungu hutolewa kwa mashetani, wala si kwa Mungu. Nami sitaki ninyi mwe na ushirika na mashetani” 1Wakorintho 10:19-20
Oneni ni pendo kuu namna gani alilotupa Baba, kwamba sisi tuitwe watoto wa Mungu! Nasi ndivyo tulivyo. Sababu kwa nini ulimwengu haututambui, ni kwa kuwa haukumtambua… Lakini mwajua ya kuwa Yeye alidhihirishwa ili aziondoe dhambi… Yeye atendaye dhambi ni wa Ibilisi, kwa sababu Ibilisi amekuwa akitenda dhambi tangu mwanzo. Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alidhihirishwa ili aziangamize kazi za Ibilisi”. 1 Yohana 3: 1-8
(Imetafsiriwa toka katika kitabu kiitwacho “Revolution in World Missions” uk. 21-22). Tafadhali pitia mtandao wao http://gfa.org

Saturday, September 30, 2017

Siku Tutakapoimba HALELUYA!


Baada ya haya nikasikia sauti kama sauti ya umati mkubwa wa watu mbinguni ikisema kwa nguvu : “Haleluya! Wokovu na utukufu na uweza ni vya Mungu wetu, kwa maana hukumu Zake ni za kweli na za haki. Amemhukumu yule kahaba mkuu aliyeuharibu ulimwengu kwa uzinzi wake. Mungu amemlipiza kisasi kwa ajili ya damu ya watumishi wake.’’

Wakasema tena kwa nguvu: “Haleluya! Moshi wake huyo kahaba unapanda juu
milele na milele.’’ Wale wazee ishirini na wanne pamoja na wale viumbe wenye uhai wanne wakaanguka kifudifudi, wakamwabudu Mungu, aliyekuwa ameketi kwenye kile kiti cha enzi. Wakasema kwa sauti kuu: ‘‘Amen! Haleluya!’’

Kisha sauti ikatoka katika kile kiti cha enzi, ikisema: ‘‘Msifuni Mungu wetu, ninyi watumishi wake wote, ninyi nyote mnaomcha, wadogo kwa wakubwa!’’

Kisha nikasikia sauti kama sauti ya umati mkubwa wa watu, kama sauti ya maji mengi yaendayo kasi na kama ngurumo kubwa ya radi ikisema: ‘‘Haleluya! Kwa maana Bwana Mungu wetu Mwenyezi anamiliki. Tufurahi, tushangilie na kumpa utukufu!

Kwa maana arusi ya Mwana-Kondoo Imewadia, na bibi arusi wake amejiweka tayari.
Akapewa kitani safi, nyeupe inayong'aa ili avae.’’ (Hiyo kitani safi inawakilisha matendo ya haki ya
watakatifu.)
- Ufunuo 19: 1 – 8

1. MAANA YA NENO HALELUYA
Kwa baadhi ya watu Neno Haleluya ni moja ya maarufu sana katika kujaribia kipaza sauti. Ikikolezwa na “Bwana Yesu Asifiwe” basi inafaa sana kwa kujaribia kama mitambo ya sauti imekaa sawa. Kwa wengine ni sehemu ya kuwalazimisha “walokole wenye masikio ya utafiti” wawasaidie katika kupata umaarufu wao. Na kwa wengine ni neno ambalo kama maneno ya kuimba yamewaishia basi ndio neno sahihi la kurefusha wimbo ili kumalizia dakika walizopewa kuimba.

Kuna ufahamu anuai juu ya neno Haleluya ambao wakati mwingine umeleta makwazo na maumivu, huku wakati mwingine ukiwapa wengine “hatua” ambazo wako tayari kuzipata kwa gharama yeyote. Vyovyote iwavyo neno Haleluya lina asili na maana yake halisi. Swali la msingi hapa si kama Haleluya inasemwa na kuimbwa namna gani bali ni nini maana ya neno hili na nani haswa anapaswa kulisema ama kuliimba!

Katika agano la Kale, ambalo kwa sehemu kubwa limeandikwa Kiebrania, neno Haleluya ni mkusanyiko wa maneno mawili “Hallelu” lenye maana “(Ninyi) msifuni” na “Yah” lenye kubeba Jina la Mungu wa Israeli, yaani Yahwe. Kwa hiyo katika matumizi yake katika agano hilo (na Biblia kwa ujumla) ina maana Msifuni (ninyi) Yahwe ikiwa ni neno ambalo linatoa amri (imperative). Katika Agano Jipya ambalo limeandikwa kwa Kiyunani, Neno hili “Alleluia” lina maana sawa na ile ya Kiebrania.


2. UZITO WA NENO HALELUYA
Wengi wamelitumia neno Haleluya vibaya. Hii ni kwa sababu ya Ujinga wa maana na uzito halisi wa neno hili. Haleluya ni Neno alilolichagua Mungu aliyeumba mbingu na dunia kama neno la amri kwa ajili ya sifa na utukufu wake. Huyu si mungu kama ilivyo miungu ya dunia hii isiyo na idadi, bali ni Mungu ambaye Uweza wote na Utukufu ni wake peke yake. Ni Mungu ambaye Hukumu zake ni za haki.

Ni Mungu aliyeona maovu ya dunia nyakati za Nuhu na akaangamiza “Kila kitu chenye uhai juu ya uso wa nchi kilifutiliwa mbali, watu, wanyama, viumbe vitambaavyo na ndege warukao angani wakafutiliwa mbali toka duniani” (Mwanzo 7:23). Ni yule ambaye aliangamiza miji ya Sodoma na Gomora na hata leo tuna ushahidi wake. Si Mungu ambaye unaweza mchezea wala kumtetea. Yeye ndiye Mungu mkuu, Muumba na Mmiliki wa vyote ikiwemo nyumba yako, ukoo wako, mali zako na uhai wako.

Hukumu za Mungu wetu ni za Haki na hapepesi macho wala kufumbia macho uovu wowote. Kama alivyoihukumu dunia ya enzi za Nuhu ndivyo atakavyomhukumu kila mmoja wetu kwa kuvunja sheria yake. Kwa wizi uwe “mdogo” wa kalamu au “mkubwa” wa ujambazi, tamaa ya macho, ulevi, uzinzi na kila ambalo Yeye kama mmiliki halali wa wanadamu wote ametukataza tusifanye. Yeye ni Yah katika Haleluya ambaye hatupaswi kulitaja jina lake bure kama sehemu ya kutafutia umaarufu, kujaribia vipaza au namna yeyote ya kulishusha jina lake. Jina lake ni kuu sana na lafaa kuheshimiwa na kila kitu na kila mtu.

Kwa hiyo Neno Haleluya linapaswa kutamkwa tu pale ambapo tunamsifu Mungu aliye hai na si vinginevyo. Kumbuka Neno hili limebeba Jina Takatifu sana la Mungu ambaye alisema wazi bila kificho “Usilitaje jina la BWANA Mungu wako bure, kwa kuwa BWANA hataacha kumhesabia hatia yeye alitajaye jina lake bure” (Kumb 5:11). Kwa hiyo ni kosa kubwa kulitumia Jina la Mungu Muumba wa Mbingu na nchi, ambaye uhai wako uko mikononi mwake, naye utakutana nae nukta moja baada ya kifo chako. Ni hatari sana, na ni upumbavu mkuu kujitia katika hatari hii.

3. HAKI YA KULITUMIA NENO HALELUYA
Kutokana na asili na maana ya neno Haleluya, sio kila mtu ana haki ya kulitamka. Biblia imeweka wazi kuwa ‘‘Msifuni Mungu wetu, ninyi watumishi wake wote, ninyi nyote mnaomcha, wadogo kwa wakubwa!’’ (Ufu 19:5). Ni watumishi wa Mungu pekee, wakubwa kwa wadogo wanaopaswa na kuruhusiwa kulitamka hili neno bila hofu ya kujiletea hatia juu ya vichwa vyao. Hii ni kwa sababu watumishi wa Mungu aliye hai ni sehemu ya Kanisa, yaani Bibi-Harusi wa Kristo ambaye ameandaliwa karamu kuu mbinguni ilhali wengine wote sehemu yao ni katika ziwa la moto.

“Kisha nikaona kiti kikubwa cha enzi cheupe, dunia na mbingu zikaukimbia uso wake Yeye aliyeketi juu yake, wala mahali pao hapakuonekana. Nami nikawaona wafu wakubwa na wadogo, wakiwa wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi na vitabu vikafunguliwa. Pia kitabu kingine kikafunguliwa ambacho ni cha uzima. Hao wafu wakahukumiwa sawasawa na matendo yao kama yaliyoandikwa ndani ya hivyo vitabu... Iwapo mtu jina lake halikuonekana katika kile kitabu cha uzima, alitupwa ndani ya lile ziwa la moto. (Ufu 20:11-15)

Kama wewe si sehemu ya Watumishi wa Mungu, basi ujue sehemu yako ni Jehanamu iwakayo moto. Je, utapata faida gani kufurahia maisha ya dhambi miaka hata mia, kama Mungu atakupa kuifikia na kisha baada ya hapo kupotelea kwenye maumivu milele? Kwa nini upotelee “Mahali ambako ‘funza wake hawafi, wala moto hauzimiki’”?

Jehanamu ipo, na wanaokwenda huko wapo (na wengine walishafika). Je huoni kama ni wakati wa kutafakari kama kweli umekubali kwa moyo wako wote kuishia motoni milele?
Pengine unajisemea kuwa huu ni upuuzi! Kama ndivyo, Neno la Mungu lina habari njema nawe. Linakwambia hivi: “Atendaye mabaya na aendelee kutenda mabaya, aliye mchafu na aendelee kuwa mchafu...” (Ufu 22:11). Kwa maana nyingine ni kuwa endelea kuponda maisha Jehanamu ya moto inakusubiria, na wakati wako utafika wala hakutakuwa na wa kukuokoa!

Kwako wewe ambaye unaona huwezi kukubali kwenda Jehanamu nina habari mbaya na kisha njema. Habari mbaya ni kuwa tayari uko njiani kwenda Jehanamu na Mungu akiamua wakati wowote kuondoa pumzi yake ya uhai aliyokupa, utaamkia kuzimu kusubiria hukumu yako ya mwisho, yaani Jehanamu ya Moto. Hauna jinsi ya kujisaidia na deni la kuvunja amri ya Mungu hauwezi kulilipa milele yote.

Habari njema ni kuwa hauna ulazima wa kulilipa wewe. Mungu katika huruma na rehema zake, aliamua kuibeba hukumu ya hatia yako yote. Katika kulitimiza hilo aliamua kuongeza uanadamu katika Uungu wake na akakaa nasi katika Utu wa Yesu Kristo. Akaishi miaka 33 bila kutenda dhambi yoyote na hivyo hakustahili kufa, maana mshahara wa dhambi ni mauti. Lakini kwa kukupenda wewe akaamua kufa akibeba adhabu uliyoistahili ili wewe uwe na Uzima alioustahili, tena uzima wa milele.

Kwa kuwa Alikuwa (na hata leo ni) Mungu, aliweza kubeba adhabu ya dunia nzima kwa kipindi kile. Kisha akazikwa na siku ya tatu akafufuka akitangaza ushindi juu ya kifo na mauti.

Deni hilo halilipwi tu kiautomatiki. Malipo yanamhusu kila anayekiri kuwa Yesu ni Bwana Mungu wake na kuwa Mungu Baba alimfufua toka kwa Wafu, na kisha kuamua kuacha njia za dhambi na kumlilia Yesu amuokoe. Basi kwake huyo deni lake litasamehewa na Jina lake litaandikwa katika kitabu cha Uzima.

Huna muda wa kupoteza kama unazitaka rehema za Mungu kabla hujachelewa. Hapo ulipo omba toba na rehema toka kwa Mungu wako aliyekuumba, Yesu Kristo. Hakuna namna nyingine ya kuepuka Jehanamu ya moto isipokuwa hii tu. Ni njia pekee ya kukufanya uwe sehemu ya Kanisa, yaani Bibi harusi wa Kristo, na kuwa na uhakika wa kuwepo katika sherehe kubwa sana ijayo huko Mbinguni. Huko tutaimba Haleluya kwa Mungu wetu, na kwa Mwanakondoo wa Mungu aliyekufa kwa mateso ili atuokoe na Jehanamu!

Naam! Utakuwa sehemu ya kile Mtume Yohana alichokisikia kuwa kuwa ni “sauti kama sauti ya umati mkubwa wa watu, kama sauti ya maji mengi yaendayo kasi na kama ngurumo kubwa ya radi ikisema: ‘‘Haleluya! Kwa maana Bwana Mungu wetu Mwenyezi anamiliki. Tufurahi, tushangilie na kumpa utukufu!

Na haitakuhitaji usubiri kufika Mbinguni ndipo uimbe haleluya, kwa sababu Bwana atakusamehe dhambi zako zote, nawe utaimba “Haleluya, wewe ni Mungu Mwokozi”. Na tena Bwana atakuongoza na kukufundisha njia ya kuiendea nawe Utasema, “Haleluya, Bwana unastahili!”. Na Yote katika Yote utagundua kuwa na utatamani kuwaambia wengine Hallelu-Yah, yaani msifuni ninyi Bwana Mungu wetu

.... Haleluya, Amen!

Sunday, April 2, 2017

Swali #4 - Maji ya kipindi cha Nuhu kutengeneza Safina yalienda wapi?

Nimekutana na hili swali likiwa limeulizwa na mwanachama wa JamiiForums. Swali lenyewe linasema hivi:

Kwa muda sasa najaribu kujiuliza hili swala kwamba Bahari ilikuwepo tangu kuumbwa kwa hii dunia ila maji yalioangamiza kizazi cha enzi za Nuhu yalipotelea wapi katika uso wa dunia au ndio kusema kina cha bahari kiliongezeka? Mwenye uelewa juu ya hili naomba anisaidie.

Nimesoma majibu mengi nikaona kuna uhitaji wa kuja na jibu ambalo ni sahihi badala ya kejeli na mashambulizi kwa muuliza swali. Swali hili sio jipya na limeulizwa kizazi hadi kizazi, na kama ilivyo ada, Biblia imeendelea kuonesha kuwa ni Neno la Mungu kwa kutoa majibu ambayo ni sahihi na yasiyobadilika licha ya uelewa wetu kubadilika.

Gharika ya nyakati za Nuhu yalikuwa ni dunia nzima kama Biblia isemavyo wazi kabisa:

" Ile gharika ilikuwako juu ya nchi siku arobaini; nayo maji yakazidi, yakaieleza safina, ikaelea juu ya nchi. Maji yakapata nguvu, yakazidi sana juu ya nchi; na ile safina ikaelea juu ya uso wa maji. Maji yakapata nguvu sana sana juu ya nchi; na milima mirefu yote iliyokuwako chini ya mbingu ikafunikizwa. Maji yakapata nguvu, hata ikafunikwa milima kiasi cha mikono kumi na mitano."
- Mwanzo 7:17 - 20

Kwa maneno rahisi ni kuwa ukiondoa Safina, hakuna kilichokuwa juu ya maji. Vyote vilifunikwa ikiwemo milima, miti, n.k. Sasa kila mwenye kufikiri atajiuliza, hayo maji yaliyofunika mpaka milima yalikwenda wapi? Maana kama ni bahari Biblia inasema zilikuwepo kabla ya gharika (Mwanzo 1: 9, 10). Kwa hiyo lazima kuna jibu kuhusu hili.

Dhahania Nyuma ya Swali
Kwa sababu swali limeulizwa katika sehemu ambayo ni ya maswali na majibu ni vyema nikachokonoa dhahania ambazo inawezekana muuliza swali na zingine toka kwa baadhi ya waliochangia ili kuweka rekodi sawa. Kwanza kuna dhahania kuwa Biblia ni hadithi na visasili ambavyo havifai kusikilizwa na watu makini. Hii ni dhahania ambayo nimekutana nayo karibu katika kila swali linalojadiliwa kuhusisha Biblia.

Kama ambavyo nimegusa katika baadhi ya maandiko yangu katika wavuti hii na katika ukurasa wetu wa Facebook, Biblia si tu iko sahihi juu ya mambo yote inayoelezea bali ni Neno la Mungu kwa wanadamu, na lenye ujumbe maalum ambao anapenda wote wausikie. Hilo tutaliangalia baadaye. Itoshe tu kusema wanaosema Biblia ni mkusanyiko wa visasili au kwamba haiwezi kuaminika, ni wale ambao aidha wana chuki au hawajafanya utafiti na kuichunguza na kuijua.

Dhahania ya pili ni kuwa sura ya nchi kabla ya gharika ilikuwa sawa na sura ya nchi ya leo. Kwamba mabonde kama Ngorongoro yalikuwapo kama ambavyo milima mirefu kama Kilimanjaro ilikuwepo. Hii ni dhahania isyo na ushahidi wowote. Kiukweli hatujui malima mrefu kuliko yote kabla ya gharika ulikuwa na urefu kiasi gani. Lakini kulingana na Biblia, japo hatujui haya yote, hii dhahania ni potofu kwa maana gharika ilibadili kabisa sura ya nchi dunia yote. Biblia inasema:

"Ikawa baada ya siku hizo saba, maji ya gharika yakawa juu ya nchi. Katika mwaka wa mia sita wa maisha ya Nuhu, mwezi wa pili, siku ya kumi na saba ya mwezi, siku ile chemchemi zote za vilindi vikuu zilibubujika kwa nguvu, madirisha ya mbinguni yakafunguka."
- Mwanzo 7:10 -11

Mistari hii hii inaonesha kuwa kulikuwa na mpasuko wa ardhi uliosababisha maji chini ya ardhi kububujika kwa nguvu. Kwa sababu hili sio andiko juu ya gharika ilivyotokea, itoshe tu kusema kuwa kupasukapasuka kwa ardhi na mabubujiko ya nguvu yalibadilisha sura ya nchi.

Kwa Hiyo Maji yalienda Wapi?
Jibu lipo katika mistari mingi ya Biblia leo nitagusia mmoja.

" Uliiweka nchi juu ya misingi yake, Isitikisike milele. Uliifunika kwa vilindi kama kwa vazi, Maji yalikuwa yakisimama juu ya milima. Kwa kukemea kwako yakakimbia, Kwa sauti ya radi yako yakaenda zake kasi, Yakapanda milima, yakatelemka mabondeni, Mpaka mahali ulipoyatengenezea. Umeweka mpaka yasiupite, Wala yasirudi kuifunikiza nchi."
 - Zaburi 104:5-9

Katika andiko hili tunaona dunia kwa ufupi. Kwamba Mungu aliiumba na baadaye kuifunika kwa vilindi kama tulivyosoma hapo juu, ambapo maji yalikuwa yakisimama juu ya milima. Sehemu ya pili inatuambia kwa "kukemea" kwake Bwana na kwa "sauti ya radi" zake yakaenda kwa kasi mpaka mahali alipoyatengenezea, na akaweka mpaka yasirudi kuifunikiza nchi.

Kwa mtu anayefahamu kuhusu elimu ya miamba (geology) atakuwa ameelewa jibu hili. Nitajaribu kulirahisisha kwa ajili ya wasomaji wangu. Lakini kujibu swali husika ni kuwa "Maji yale yapo, ila yalihamishwa na kuwekwa mahali, hapa hapa duniani".

Gharika kubwa kama ya nyakati za Nuhu lazima isababishe mvurugano na mtitiriko wa nguvu wa maji mengi. Athari za maji kutiririka kwa namna hii huwa ni kusawazisha sehemu nyingi zilizoinuka hasa kwa maji yaliyodumu siku mia hamsini. Kwa hiyo lazima kukemea huku na radi hizi inamaanisha tukio la nguvu ambalo lilisababisha maji kuanza kutembea kwa kasi mpaka yalipofika mahali yalipowekwa hata leo.

Wanasayansi wa Kikristo wamefanya tafiti mbalimbali kujua kama wanaweza kujua angalau namna na mahali yalipo maji hayo. majibu ya tafiti hizi ni kuwa Bwana Mungu alifanya jambo ambalo lilisababisha kubonyea kwa gamba la dunia (earth's crust) na kusababisha sakafu ya bahari kushuka chini na upande mwingine wa ardhi kupanda juu. Hivyo maji yakashuka huko na mpaka leo yapo huko baharini.

Matokeo haya yanakubaliana na ushahidi tulio nao. Kwa mfano juu ya mlima mrefu kuliko yote, Everest katika safu za milima himalaya, yamekutwa matamahuluku. Kwa hali ya hewa ya milima kama hii hatutarajii kuyakuta. jibu rahisi ni kuwa milima ukiwamo Everest ni matokeo ya matendo ya Mungu yaliyosababisha kuinuka kwa ardhi kuelekea mwishoni au baada ya gharika.

Lakini pia dunia ikiwekwa ulazo, maji yaliyopo yanatosha kuifunika yote kwa kilomita 1.7 - 3 kwa makadirio ya watafiti. Kwa hiyo Mungu aliibadili sura ya nchi na hivyo kuyahamisha maji yale.

Kwa kumalizia nikuulize swali. Ulishawahi kujiuliza kwa nini Mungu aliiangamiza dunia kwa gharika? Hilo ni swali la msingi sana na ningependa nikujibu. Ni kwa sababu uovu ulikuwa mwingi sana. Je waonaje leo? Uovu ni mwingi pia. Basi siku inakuja ambapo Mungu atawahukumu walio wafu na walio hai. Kila dhambi iwe ni uongo, wizi (hata wa pipi), uasherati, tamaa, chuki na nyinginezo zote zitahukumiwa.  Kama uliwahi kutenda dhambi hata moja tu maishani mwako, uko hatarini. Atakapohukumu utakuwa upande wa maumivu.

Lakini Yesu alikufa na kubeba dhambi ya ulimwengu wote, na ni Yeye pekee anaweza kukusamehe dhambi zako na kusimama kama wakili na mtetezi siku ile ya kutisha. Mwamini leo, tubu dhambi zako mbele zake. Geuka na kuacha njia mbaya na umtumainie Yesu pekee kwa wokovu wako hata siku ile. Kumbuka Biblia inasema:

" Kisha nikaona kiti cha enzi, kikubwa, cheupe, na yeye aketiye juu yake; ambaye nchi na mbingu zikakimbia uso wake, na mahali pao hapakuonekana. Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi; na vitabu vikafunguliwa; na kitabu kingine kikafunguliwa, ambacho ni cha uzima; na hao wafu wakahukumiwa katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao..... Na iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto." - Ufunuo 20:11-15

Wednesday, January 11, 2017

Swali #3 - Je Kuna uhusiano kati ya sayansi na Mungu?

Swali hili limeulizwa na msomaji wetu likiwa na sehemu mbili ambazo zinafanana:
  1. Je kuna uhusiano kati ya Mungu na Sayansi?
  2. Je Ukweli ni upi kati ya binadamu alikuwa nyani na kutoka kwa Adamu na Eva?
Jibu: 
Ni vema kabla ya kujibu haya tukaweka sawa tafsiri za maneno ili  yanapotamkwa wote tuwe na uelewa mmoja wa maneno hayo.  Sayansi imetokana na neno la  Kilatini "scire" lenye maana Fahamu. Mnyumbulisho wake, yaani "scientia" (ufahamu) ndilo limezaa neno sayansi. Kifupi Sayansi maana yake ni ufahamu. Mungu, kwa upande mwingine ni Yeye aliye mkuu kuliko wote, asiye na mwanzo bali Mwanzo wa vyote na asiye na mwisho ila ni Mwisho wa vyote. Hii ni tafsiri fupi ambayo haisemi kila kitu kuhusu Mungu, lakini inatosha kwa mada yetu hii. Kwa hiyo kimsingi swali la msomaji wetu ni kuwa "Je kulingana na ufahamu tulionao (sayansi) je kuna Mungu aliyeumba Adam na Hawa au tulibadilika toka viumbe wengine"? Jibu nitalitoa hapo chini, kwa sasa tuangalie pande mbili za Swali.

1. Je Kuna Tunafahamu kuwa kuna Mungu? Kama Yupo, Anahusianaje na Sayansi?
Hili ni swali la msingi ili kabla ya sehemu ya Pili. Biblia inatuambia "hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi" (Mwa 1:1) na Tena inatuambia Warumi 1:20 inatuambia kuwa sote tunajua ya kuwa Mungu yupo na hatuna udhuru.

 "Kwa sababu mambo yake [Mungu] yasiyoonekana tangu kuumbwa ulimwengu yanaonekana, na kufahamika kwa kazi zake; yaani, uweza wake wa milele na Uungu wake; hata wasiwe na udhuru
- Warumi 1:20 (msisitizo ni wangu)

Kama ni kweli basi yapaswa kuwepo na mambo yanayoonyesha wazi kuwa kuna Mungu. Yafuatayo ni Mambo mawili kati ya mengi sana, ambayo yanathibitisha ukweli wa andiko hili na kuonesha uhusiano wa sayansi na Mungu. Kumbuka, hivi si vipimo vya uwepo wa Mungu, bali ni alama (fingerprint) alizoacha makusudi ili kila anayemtafuta ajue Yupo!

i. KANUNI YA ULINGANIFU, SAYANSI NA MUNGU
Ili sayansi iweze kufanya kazi lazima kuwe na ulinganifu (uniformity). Sayansi kamwe haiwezekani kama vitu vinakwenda ovyo ovyo. Mfano huu utakuonesha mazingira ambayo hakuna ulinganifu. "Gari lilikuwa inakwenda 100km/saa kwa saa kisha bila kuguswa wala mazingira kubadilika likaanza kurudi kinyume nyume kwa 120km/saa halafu ghafla likapaa na halikurudi tena". Unaweza kucheka lakini huu ndio ukweli, bila ulinganifu hakuna sayansi maana inawezekana leo unachanganya kemikali A na B zinatoa C na kesho unachanganya kemikali A na B katika mazingira yaleyale unapata X. Ili Sayansi iwezekane inahitaji kuwe na ulinganifu.

Swali la msingi linakuja hapa: Kwa nini kuna ulinganifu na si shaghala bhagala? Je ni nani/nini aliyeweka kanuni ya ulinganifu na kuisimamia? Biblia ipo wazi kuwa ni Mungu ambaye anavishikilia vitu pamoja na ameamuru viende kwa ulinganifu.

"Muda nchi idumupo, majira ya kupanda, na mavuno, wakati wa baridi na wakati wa hari, wakati wa kaskazi na wakati wa kusi, mchana na usiku, havitakoma."
- Mwanzo 8 : 22

Hapa tunaona kwamba ni Mungu mwenyewe ndiye aliyeamuru kuwe na ulinganifu. Tuna uhakika mwakani kutakuwa na masika tena kwa sababu Mungu alituahidi itakuwa hivyo. Lakini si hivyo tu. Mungu ndiye anayashikilia mambo yote ili yakapate kuwa na ulinganifu. Biblia tena inatuambia:

" ... akivichukua vyote kwa amri ya uweza wake (upholding all things by the Word of His power)" - Ebr 1:3

Je kuna Mungu? Jibu ni ndio. Ulinganifu tunaouona hauwezekani kama hakuna Mungu. Vinginevyo lazima ueleze ni kwa nini vitu vina ulinganifu badala ya shaghala bhagala. Je kuna uhusiano wa Sayansi na Mungu? Ndio! Mungu anaweka sheria za msingi za Sayansi na kufanya tuwe na uwezo wa kujua mambo yote tunayojua. Hapa nimejadili kanuni/sheria moja tu. Mungu akitupa Neema basi tutajadili nyingine.

ii. TUNAJUAJE TUNAYOJUA KUHUSU TUNAVYOVIJUA?
Ulishawahi kujiuliza hili swali? Mara nyingi tunaongea mambo na kudhania tunajua. Lakini huwa hatujiulizi swali, tunajuaje? Mfano ni mtu anaposema "haki haikutendeka". Anajuaje kilicho haki na kuwa haikutendeka? Haki sio kitu kama nyanya ambacho unaweza kukiona au kukigusa. Mfano mwingine ni hesabu. Hatuwezi kugusa hesabu wala kuziona. Lakini huwa"tunajua" hesabu. Mifano ipo mingi ila swali la msingi ni kuwa tunajuaje tunavyojua?

Kila mtu ana mtazamo ambao kimsingi ni namna anavyotafsiri matukio mbalimbali ya dunia hii. Mtazamo unajengwa na vitu ambavyo huwezi kuvithibitisha, ila unaamini ni kweli. Kwa maana nyingine, mitazamo yote imejengwa kwa kuamini. Kwa mfano, wote tunakubali kuwa lazima tuwe na uongozi, na kwa hakika tuna viongozi. Lakini ni kwa nini lazima tuwe na viongozi? Unaweza kutaja faida za kuwa na viongozi. Hii haitoshi kwa sababu kuna hasara pia za kuwa na viongozi. Na zaidi faida za uongozi sio sababu ya ulazima wa kuwa na uongozi. Hii ni sehemu ambapo mtazamo wa mtu unaingia.

Watu wanaweza kuwa na ushahidi uleule lakini jinsi watakavyoutafsiri itategemeana na mtazamo wao juu ya dunia. Dunia tuliyo nayo ni ileile. Ila kuna wanaosema imekuwapo kwa maelfu ya miaka na wengine wanasema imekuwapo kwa mamilioni ya miaka. Mtazamo ni kama lensi za miwani. Mtu aliyevaa miwani yenye lensi nyekundu, ataona vitu kwa rangi isiyo sawa na aliyevaa myeupe au ya kijani. Vitu vyeupe ataviona ni vyekundu.

Mtazamo ni mada inayojitegemea, ila kwa sasa itoshe kukupa mwanga. Tukirudi katika mada husika, kuna mitazamo miwili. Hii si mitazamo pekee, ila ni mitazamo inayotawala katika mada ya Mungu na sayansi. Mtazamo wa kwanza ni ule wa nadharia ya mageuko (evolution theory) na ule wa Uumbaji (creationism). Hebu tuangalie kwa ufupi misingi ya mitazamo hii.

Nadharia ya mageuko inasema hivi. Kulikuwa na nukta moja iliyokuwa imegandamizwa sana. nishati, maada na nafasi vyote vilikuwa katika nukta hii. Kisha ukatokea mpasuko mkubwa, ile nukta ilipasuka; Na katika mpasuko huo mabonge ya moto yalisambaa, miaka yapata bilioni 13.4 iliyopita. Kwa miaka milioni nyingi, mabonge haya yaliendelea kupoa na baada ya muda, katika moja ya bonge hilo kulianza kunyesha mvua na kutengeneza bwawa la kemikali mbalimbali. Kwa miaka mamilioni ya mchanganyiko katika "supu" hii, kukatokea kiumbe hai cha seli moja. Kufanya hadithi iwe fupi seli hii moja ilipitia hatua za mageuko kwa mamilioni ya miaka na kutoa aina mbalimbali ya viumbe hai tuvionavyo leo. Hakuna Muumbaji kwa watu wa mtazamo huu na vitu vyote ni sawa. Hakuna tofauti ya wewe na ndege kwale kiuhalisia. Wote ni wanyama tu.

Kwa upande mwingine, wale wa upande wa Uumbaji, wao wanaamini kuwa hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi na vyote vilivyomo (Mwa 1:1). Kwamba kumekuwa na mabadiliko ndani ya aina za wanyama. Mbuzi ameendelea kubadilika kuwa mbuzi na mbwa akiwa mbwa. Mbwa mkubwa, Mbwa mwitu ... lakini ni mbwa. Hakuna mageuko ya kutoka aina moja kwenda nyingine, katika mtazamo huu. Mwanadamu ameumbwa maalum kwa mfano wa Mungu na hivyo ni tofauti na viumbe wengine wa Mungu duniani.

Sasa tukirudi kwenye swali la msingi, tunajuaje tunavyojua? Kwa upande wa mtazamo wa mageuko hakuna namna ya kujua. Kwa ukweli kabisa hakuna kujua wala kutojua. Kama sisi ni matokeo ya muunganiko wa kemikali, basi mwanadamu si zaidi ya kemikali. Kinachoendelea katika ubongo wangu ni mipambano ya kemikali na kama mipambano hiyo itaamua kuwa 2+2=3 hakuna tatizo kwa sababu kemikali katika ubongo wako zaweza kuamua 2+2=6. Kama ubongo ni mpambano wa kemikali na umeme basi hakuna anayekosea. Lakini tunajua kuwa kuna kujua na kutojua na kuna ukweli na uongo. Kwa hiyo nadharia si sahihi na imeshindwa kueleza kwa nini tunajua tunavyojua.

Kwa upande wa Uumbaji hili ni suala rahisi. Mwanadamu ni nafsi hai (Mwa 2:7) ambaye ameumbwa kwa mfano wa Mungu (Mwa 1:26-27). Kwa hiyo Mungu ameweka katika mwanadamu uwezo wa kuwaza, na kuwa na utashi wa kuamua. Mwanadamu sio kemikali za Ubongo tu bali kuna sehemu ambayo haionekani kwa macho. Kwa sababu hiyo kuna kujua na kutojua, uongo na ukweli. Mungu ndiye anayesema kipi ni kweli na kipi ni uongo, na ndiye Mkuu katika yote.

JUMLA YA YOTE
Mada hii ni pana sana, na hapa nimegusa chembe tu, nikigusa sehemu chache kwa kifupi sana. Kwa kukazia niliyokwisha kuyasema ni kuwa, uhusiano wa Mungu na sayansi ni kuwa Mungu ndiye muumbaji wa vyote. Ndiye aliyeweka sheria/kanuni zinazosimamia maumbile na uumbaji ambazo sisi tunatafuta kuvijua. Sayansi ni kujua yale ambayo Mungu ameyaweka. Hakuna ushahidi uwao wowote wa kuonyesha ukweli wa nadharia ya mageuko. Na kwa sababu nadharia hii imekuwa mtazamo kwa wengi basi kila ushahidi wanautafsiri kwa lensi za mageuko.

Hakuna mgongano kati ya Mungu, Neno lake (Biblia) na Sayansi.

NUKUU ZA ZIADA
Hawa ni wanasayansi wachache walioamini uwepo wa Mungu na uhusiano wake na sayansi.

"Huu mfumo wa kupendeza kuliko yote wa jua, nyota sayari na vimondo, unaweza kutokea tu kutoka kwa maamuzi na utawala wa mtu Mtu mwenye akili na nguvu."
- Isaac Newton (Mwana mahesabu, Mnajimu, mwana fizikia, mwanasayansi mwenye ushawishi kuliko wote nyakati zote).

 "Kitabu cha asili ambacho lazima tukisome kimeandikwa na kidole cha Mungu"
- Michael Faraday (Mwanasayansi na mtaalam wa mambo ya usumaku na umeme-kemikali. Mmoja kati ya wanasayansi mahiri kabisa wa wakati wote)

"Fundisho la kuwa vitu kujiumba kwa vitu halitapona kutoka katika pigo la mauti lililoletwa na jaribio hili dogo"
- Louis Pateur (Mwana kemia na baiolojia ya viumbe wadogo. Mgunduzi wa kanuni za chanjo na mengine)

Kama una swali tutumie kwa anuani Yetu hii. Pia usiache kusome kipande kifupi cha Yesu Kristo

Saturday, May 2, 2015

Swali #2 Melkizedeki ni Nani?

Swali hili limekuwa likijirudia kwa karne nyingi sasa, na nadhani ni wakati sahihi, kama walivyofanya Wakristo wengine karne zilizopita, nikaweka mchango wangu wa uelewa wangu juu ya Biblia. Baada ya kujifunza toka kwao na kuyachunguza maandiko binafsi, nina hakika kuwa mchango wangu huu utawasaidia wenye kiu ya kujua Neno la Mungu zaidi. Usijekosea ukadhani ninajua kila kitu au ya kuwa nina "upako maalum", la hasha! Neno la Mungu linatufundisha kuwa Wanafunzi wa Neno, tusio na sababu ya kutahayari (2Tim 2:15). Kwa hiyo kama ulivyo ndivyo nilivyo na ndivyo tulivyo: wanafunzi wa Bwana Yesu.

Baada ya utangulizi huu, hebu na tuliangalie swali husika: Melkizedeki ni nani?

Kulingana na Program ninayotumia kujifunzia, neno Melkizedeki limeonekana katika Biblia mara kumi (Mwa 14:18, Zab 110:4, Kitabu cha Waebrania - 5:6, 5:10, 6:20, 7:1, 7:10, 7:11, 7:15, 7:17). Tatizo kubwa katika kumfahamu huyu mtu ni kuwa anaibuka kama mvuke na kuyeyuka kama barafu, hivyo kuna mengi ambayo inakuwa vigumu kuyafahamu kwa hakika. Ili kuchanganua vema nimeligawa jibu katika sehemu kuu tatu: tunachokijua, kilicho na utata na mtazamo wangu.
(a) Tunachokijua kuhusu Melkizedeki

Mwanzo 14:18, bila taarifa ya kabla inamleta katika picha Melkizedeki. Hebu tuone tunapata nini katika andiko hili:
Abramu aliposikia ya kwamba nduguye ametekwa mateka, akawapa silaha vijana wake, waliozaliwa katika nyumba yake, watu mia tatu na kumi na wanane, akawafuata mpaka Dani.   Akajipanga apigane nao usiku, yeye na watumwa wake, akawapiga, akawafukuza mpaka Hoba, ulioko upande wa kushoto wa Dameski.  Naye akarudisha mali zote, akamrudisha na Lutu nduguye na mali zake, na wanawake pia, na watu.  Abramu aliporudi kutoka kumpiga Kedorlaoma na wale wafalme waliokuwa pamoja naye, mfalme wa Sodoma akatoka amlaki katika bonde la Shawe, nalo ni Bonde la Mfalme.  Na Melkizedeki mfalme wa Salemu akaleta mkate na divai, naye alikuwa kuhani wa Mungu Aliye juu sana.  (Mwa 14:14 - 18)

Tunaona sifa mbili za Melkizedeki, kwanza mfalme na pili ni kuhani wa Mungu aliye juu. Salem ndiyo eneo ambalo mfalme huyu alitawala kulingana na mstari huu.  Salem ina maana ya amani. Kwa hiyo Melkizedeki alikuwa mtawala wa sehemu yenye jina lenye tafsiri ya amani. Akiwa kama kuhani, anambariki Ibrahimu na anapokea zaka za Ibrahimu  (mst 19-20).

Baada ya kitabu cha Mwanzo, jina la Melkizedeki tunalikuta Zaburi 110:4. Kabla hatujaiangalia Zaburi hii ni vyema machache yakasemwa juu yake. Mwandishi wa zaburi hii ni Daudi na anaiandika kama "Neno la Bwana kwa Bwana wangu". Bwana wa kwanza wa Daudi anamwambia Bwana wa pili, katika mistari saba ya zaburi hii. Na sehemu ya maneno ya Bwana kwenda kwa Bwana ni yale ya mstari wa nne ambayo ndiyo tutayaangalia kwa sasa:
Bwana ameapa, Wala hataghairi, Ndiwe kuhani hata milele, Kwa mfano wa Melkizedeki (Zaburi 110:4)

Kwa hiyo Bwana anaambiwa na Bwana kuwa yeye ni kuhani (sio atakuwa kuhani), mfano wa Melkizedeki. Neno mfano wa ni dibrâh  ambalo lina maana ya "utaratibu wa kufuata" au "namna ya". Kwa hiyo Bwana ni kuhani kwa mpangilio au utaratibu uleule wa Melkizedeki, mfalme wa Salem. Ingawa hakuna mengi sana tuyapatayo hapa kuhusu Melkizedeki, ila machache tunayapata.

Moja ni kuwa Melkizedeki sio mfano au roho, ila ni mtu halisi. Hii inatufanya tujue kuwa Mwanzo 14:18 inaongelea historia na si mfano kutoka hewani. Lakini pia ukuhani wake ni halisi na sio aina fulani ya mfano usio halisi (abstract title).

Hizi ndizo sehemu mbili pekee ambazo tunaziona katika Agano la kale. Sasa na tuangalie kitabu pekee cha agano jipya kinachotuambia habari za Melkizedeki. Sehemu ya kwanza jina Melkizedeki liaonekana katika agano jipya ni Ebr 5:6 amabapo ni nukuu ya Zab 110:4 ikitupa majibu ya Bwana anayeambiwa na Bwana kuwa ni Yesu Kristo. Hicho ndicho tunachokipata katika mstari huu. Mstari wa 10 sura hii hii unatupa picha ya Melkizedeki kuwa hakuwa kuhani wa kawaida, bali kuhani mkuu. Sura 6:20 inarudia kusisitiza kile sura ya 5:6 kinasema, kuwa, Yesu ni kuhani mkuu mfano wa Melkizedeki.

Sura ya saba inatupa historia ya Melkizedeki kwa kina kidogo kuliko Zaburi 110 na Waebrania 5 na 6. Haya ni mambo tunayoyapata sura ya 7:1-17:
  • Melkizedeki ni halisi kama alivyokuwa Ibrahimu 
  • Maana ya Jina Melkizedeki ni mfalme wa haki na Salem maana yake ni amani
  • Alikuwa kuhani aliyepokea zaka, ukuhani wake ni tofauti na ule wa Walawi

Kwa hiyo tunajua bila shaka kuwa Melkizedeki alikuwa ni mtu halisi na sio kisasili, na alikuwa kuhani mkuu. Melkizedeki ni jina lenye maana ya Mfalme wa haki, tena Mfalme wa salem ina maana ya Mfalme wa amani.

Baada ya kuyaona yale yaliyo bayana na tuhamie sehemu ngumu yenye mawazo mgawanyiko juu ya utambulisho na asili ya Melkizedeki.
(a) Utata wa Utambulisho wa Melkizedeki na Mtazamo wangu

Kwa sababu Katika kitabu cha Mwanzo hatuna maelezo ya kutosha kumhusu huyu mtu, tutategemea sana Waraka wa Waebrania kujua juu ya utambulisho wake. Kumbuka kuwa mwandishi wa kitabu hiki ni Myahudi mzuri ambaye alikuwa na nafasi ya kusoma maandiko ya kihistoria ya Wayahudi ambayo leo hatuna baada ya hekalu kuchomwa moto. Hivyo basi lazima katika kusoma kwetu tusijifanye kujua kuliko mwandishi bali tujaribu kwa kadri ya uwezo wetu kuelewa alichomaanisha mwandishi.

(i) Nini Mwanzo wa Melkizedeki?
Kuna mawazo ya aina mbili hapa. La kwanza ni kuwa Melkizedeki alikuwa mwanadamu na mfalme wa Salem. Wengine (nikiwemo mimi) huamini kuwa maelezo ya Biblia kuhusu Melkizedeki yanabeba vitu ambavyo mwanadamu hawezi kuwa navyo. Mathalani Ebr 7:3 inatuambia kuwa yeye hana baba wala mama naye ni kuhani milele. Wandugu wanaotafsiri kuwa ni mwanadamu hudai kuwa andiko hili lina maana ya kuwa kumbukumbu zake kuhusu uzao na wazazi wake hazipo na kwamba umilele wa ukuhani wake ni kuweka mkazo na si vinginevyo.

Binafsi naona msimamo huu una mapungufu mengi sana. Kwanza Biblia iko wazi kuwa hana wazazi (na sio hana kumbukumbu ya wazazi) na kuonesha hilo imeweka wazi kuwa hana baba wala mama. Lakini kuonesha sio mwanadamu maandiko yameweka wazi kuwa " hana mwanzo wa siku zake, wala mwisho wa uhai wake"  Kwa maana nyingine ni kuwa amekuwapo siku zote na uhai wake upo ndani yake Mwenyewe.

(ii) Melkizedeki ni Nani?
Baada ya kuona maandiko yanasema nini juu ya Melkizedeki ni wakati wa kuvumbua utambulisho wake. Kwa kuwa Mtu huyu hana mwazo wa siku wala mwisho wake (wa milele), kama ulivyo ukuhani wake, basi yeye ni Mungu. Ni Mungu peke yake ndio hana mwanzo wala mwisho. Pia ni Mungu pekee uhai wake uko ndani yake, na hivyo kwa kuwa hana mwanzo wala mwisho vivyo hivyo na uhai wake!

Yohana 1 inatuelezea habari za Neno nayo inasema "Ndani yake ndimo ulimokuwa uzima" (mst 4) na Yoh 1:1 inaweka wazi kuwa kabla ya Mwanzo neno alikuwepo. Kwa hiyo kwa kwa uelewa wangu wa Biblia Takatifu ni kuwa Melkizedeki ni Mwana wa Mungu kabla hajauvaa mwili na kuitwa Yesu. Hii sio mara ya kwanza kwa Kristo, Masihi (Bwana wa pili katika Zab 110), kuwatokea  wanadamu katika mwili. Alimtokea Ibrahimu akiwa na malaika wawili (Mwanzo 18)

(iii) Vipi wanaoamini Melkizedeki ni mwanadamu?
Kama ni swali la kuhusu tafsiri yao, ninaamini wanakosea kutafsiri maandiko. Lakini kama ni swali la kama wanakwenda mbinguni au motoni jibu ni kuwa haihusiani na safari hii. Kuna watu hawajui hata habari za Melkizedeki a tutakutana nao mbinguni na wengine wanajua kwa usahihi lakini, kwa huzuni, watakwenda Jehanamu. Hii ni kwa sababu njia ya kwenda mbinguni si kujua juu ya Melkizedeki au mtu mwingine yeyote bali ni kutubu dhambi zako mbele za Mungu na kumwamini Yesu Kristo na kazi aliyofanya pale msalabani kulipa deni ya dhambi yako. Hii ndio tofauti ya waendao mbinguni na Jehanamu: Yesu Kristo!

Kwa hiyo, kama una elimu sahihi juu ya tafsiri ya biblia, jua haitakusaidia kama dhambi zako hazijasamehewa bado. Utubu sasa na kumwamini Yesu kama Bwana na Mwokozi wa maisha yako. Nani ajua kuwa maneno haya yanaweza kuwa ya mwisho kuyasoma kabla hujapita mlango wa mauti kukutana na Mungu wako?
"Kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka." (Warumi 10:9)