Pasaka Ina Maana Gani Kwako?
Moyo huu wa pasaka una sura mbili. Sura
ya kwanza ni ya tabasamu la bibi harusi akimsubiri Bwana harusi arudi
mara amalizapo kujenga nyumba watakayokaa huko kwa Baba wa Bwana
harusi. Bibi harusi anasubiri kwa hamu akichungulia chungulia aone
kama Bwana wake yuaja. Akijiandaa na kuhakikisha yu msafi ili sekunde
ile Bwana harusi atakayokuja amkute tayari. Sisi kama kanisa la
Kristo, ambao tumemkiri na kumwamini Yesu awe si tu Mwokozi kwetu
bali mtawala wa maisha yetu na bosi mkuu, tunaitwa ni bibi harusi,
ambapo tunapaswa kuishi kwa utakatifu kama "bikira safi"
(II Kor 11:2). Na ndipo tunasubiri siku ile ambapo tutasahau taabu na
maumivu, na magonjwa na yote ya dunia hii, siku ile kuu ya kukutana
na Bwana harusi, maana:
"Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza. Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele" (1Th 4:16 - 17)
Picha ya pili ni ya huzuni, mashaka na
kukosa amani. Amini usiamini, pamoja na Mungu kuingia gharama ya
kulipa deni la dhambi kuna watu wako wanaugulia maumivu Kuzimu, na wapo kati
yetu, pengine hata ikawa ni wewe unayesoma, ambao wataingia Jehanamu
ya moto. Kiburi cha kutotaka kushuka mbele za Muumba wako na kupenda
kwako dhambi vitakuangamiza. Kwako mtu wa namna hii pasaka ni ujumbe
wa machozi na majonzi.
Ina maana kuwa Yesu atakapokuja
kuchukua bibi arusi wake, hautakuwa mmojawapo. Ni kweli unajidanganya
kuwa wewe ni Mkristo huku ukijua toka katika moyo wako kuwa Yesu
hakujui. Ndio, endelea kujifariji ila siku yaja ambapo Yesu anasema
"Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni
kwangu, ninyi mtendao maovu" (Matt 7:23). Usisherekee Pasaka
maana moyo wa pasaka kwa watu wa aina yako ni tangazo la ole!
Si kwamba tu utakosa nafasi ya bibi
arusi, lakini pia utapitia wakati mgumu sana duniani ikitokea ukawa hai. Mungu
atauhukumu ulimwengu kwa dhiki kubwa sana ambayo haijawahi kuwepo
wala baada ya hapo haitakuwapo. Itakuwa ni zaidi ya vita zote mbili
za dunia. Na mwisho Yesu huyu ambaye tunasherekea pasaka leo ataweka
kiti cha Enzi cha hukumu ili akuhukumu kwenda ziwa la moto, naam "Na iwapo mtu ye yote
hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile
ziwa la moto" (Ufu 20:15). Mpaka sasa sijaelewa unasherekea nini
katika hali kama hii!
Ndio, sitaki nikufariji kwa maneno mfu
maana Biblia iko wazi kuwa "Kwa maana [Mungu] ameweka siku
atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye
amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu"
(Mdo 17:31), ufufuo wa Yesu ambao unapanga kuusherekea ni uthibitisho
kuwa utahukumiwa na Mungu kwenda ziwa la moto hakika, ni kipi cha
kusherekea kwako?
Ushauri Mwema
Kwako wewe uliye kati ya bibi arusi,
jiweke safi. Tengeneza mavazi yako ili akija sasa, uwe tayari kwenda
nae kwa Baba yake. Kumbuka atakuja kuchukua kanisa safi, lisilo na
makunyazi wala mawaa. Yesu Kristo anakuja!
Kwako wewe usiyeokoka, fanya hima
ufanye amani na Muumba wako. Maana "ukimkiri Yesu kwa kinywa
chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu
alimfufua katika wafu, utaokoka" (Rum 10:9). Unasema utafikiria?
Hujui kama muda huu unaposoma hapa unaweza kuwa umebakiza dakika au
hata sekunde chache kumaliza maisha yako? kumbuka baada ya kifo ni
hukumu (Ebr 9:27). Fanya Uamuzi wa busara sasa. Chagua kuokoka na
hasira ya Mungu ili pasaka iwe ni tabasamu kwako. Kwamba tutakaa na
Mungu milele, ndio kusudi la Mungu na moyo wa pasaka!
Mungu akutunze na kukubariki!
Stefano