Friday, April 18, 2014

MOYO WA PASAKA - Sehemu ya I

Kwa wengine pasaka ni wakati wa mapumziko ya kifamilia na kutafakari maendeleo yao, walipojikwaa na wanapoelekea. Kwa wengine ni Wakati wa "kuponda mali, kufa kwaja" na wapo ambao pasaka ni wakati wa kufikiria kuhusu dini zao na kuangalia namna wanayoweza kujitengenezea mazingira ya kuzikwa na dini zao wakifa. Lakini kwa wengine pia ni wakati wa kusherekea ushindi wa Bwana na Mwokozi wao, Yesu Kristo.

Makundi yote haya, isipokuwa la mwisho, hawako sahihi. Pasaka ni wakati mzuri wa kusherekea ushindi wa Mwokozi wetu Yesu Kristo. Hili ni jambo la muhimu sana ambalo bila hilo hakuna Pasaka. Swali la msingi ambalo nilikuwa nalitafakari hata kunisukuma kuandika makala hii fupi sana ni hili "nini hasa moyo wa Pasaka"? Ni kweli ni siku ya kufurahia ushindi, na ni kweli kuwa Ukombozi wa Mwanadamu hautenganishwi na tukio hili. Lakini ni nini moyo wa Pasaka hasa? Majibu ya tafakari hii ndiyo ninataka nikushirikishe.

Mfululizo wa Matukio
Kabla sijaweka kile nimejifunza leo hebu tuangalie kifupi matukio kuelekea pasaka. Yesu na wanafunzi wake wako katika chakula cha jioni, huku shetani akiwa amekwisha uteka moyo wa Yuda. Yesu hali akijua anahesabu masaa kabla ya kipigo, maumivu na mateso, anawafundisha wanafunzi wake kutumikiana, akifanya kazi iliyofanywa na watumwa, kuosha miguu ya wanafunzi wake. Petro anajaribu kuzuia hili (Yoh 13:6-9) Bwana anamkemea na kuendelea na kazi yake hiyo. Mwisho Yesu anawaambia wanafunzi kuwa Yuda Iskariote atamsaliti na Yuda, kwa kuingiwa na shetani, anakwenda zake kulifanya alilo kusudia moyoni mwake. Haya yote ni mfululizo wa matukio kuelekea Pasaka, sura ya 13. Baada ya haya yote, inafuata sura ambayo ina moyo hasa wa Pasaka!

Moyo wa Pasaka na kusudi la Mungu
Moyo wa pasaka umeambatana na kusudi la Mungu la milele. Kabla hajaumba chochote, Mungu alijua mambo yote ambayo yatatokea katika historia ya mwanadamu. Kwa sababu ya ufahamu wake wa milele, usio na mwisho, Mungu aliumba akiwa na kusudi. Kusudi hili ndio moyo wa Pasaka. Kifo cha Yesu Kristo, na kufufuka kwake, vyote hivi ni njia za kufikia kusudi hili: Mahusiano ya Mungu na mwanadamu. Hebu tusome maneno ya Yesu mwenyewe katika sura hii ya 14 ya Yohana:
"Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi. Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo" (Yoh 14:1 - 3)
 
Yesu anawaambia wanafunzi wake kuwa wasifadhaike, na sababu ni kuwa anakwenda kuwaandalia mahali katika makao ya mbinguni. Mstari huu unatupa moyo wa pasaka ni Mungu akae na wanadamu. "Maana naenda kuwaandalia mahali", ni ahadi nzito kabisa kuwa ipo siku inakuja ambapo wote tulio wanafunzi wa Yesu Kristo tutakaribishwa naye kwa Baba yake. Ndiyo, Yesu Mwenyewe anasema "nitakuja tena niwakaribishe kwangu". Huu ndiyo moyo wa Pasaka.

Mungu alipomuumba mwanadamu, alikuwa na ushirika naye wa namna ya ajabu kabisa. Hata pale Adamu na mkewe walipoasi sheria ya Mungu bado Mungu aliwatembelea. "Kisha wakasikia sauti ya Bwana Mungu, akitembea bustanini wakati wa jua kupunga" (Mwa 3:8). Mungu alimuumba Mwanadamu ili awe na ushirika nae, na ndio maana akamuumba kwa mfano Wake na sura Yake (Mwa 1:26-27). Kwa sababu ya kusudi hili Mungu alitembea na Henoko miaka 300 (Mwa 5:22), Nuhu, Ibrahimu, Daudi na wengine wengi. Ibrahimu, Biblia inatuambia, " alikuwa akiutazamia mji wenye misingi, ambao mwenye kuubuni na kuujenga ni Mungu" (Ebr 11:10). Ni Mji huu ambapo Mungu atakamilisha kusudi lake la milele, ambapo "maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu" (ufu 21:3).

Yesu anaongelea makazi haya ambayo kwa milenia mbili amekuwa akituandalia, ili alipo nasi tuwepo. Huu ndio moyo wa Pasaka. Mungu aliamua kumtoa mwanawe wa pekee ili afe, ili kwa kifo chake Yeye asiye na hatia, abebe hatia zetu zote na tuweze kuwa na uhalali kwa kifo na damu yake, kuingia katika mji huu. Mauti ya msalaba na ufufuko wa Yesu ulikuwa ni kutimiza kusudi hili na ndio moyo halisi wa pasaka!

Katika sehemu ya pili tutamlizia kuona kwa nini na jambo hili lina maana gani kwako.
Amani ya Kristo, na Neema yake kuu iwe nawe, amen!
Stefano

Soma Sehemu ya Pili hapa


No comments:

Post a Comment