Saturday, May 3, 2014

Swali #1 – Je Daniel Alikosea Jina la mfalme wa Mwisho wa Babeli?


Swali
Danieli Sura ya Tano inasema Belshaza ndiye alikuwa mfalme wa mwisho wa Wakaldayo. “Usiku huo huo Belshaza, mfalme wa Wakaldayo, akauawa. Na Dario, Mmedi, akaupokea ufalme, naye umri wake alikuwa na miaka sitini na miwili.” (Dan 5:30-31). Katika maandishi ya wanahistoria wengine haiko hivyo na kutoka katika maandiko ya kale tunajua kuwa Nabonidus ndiye alikuwa mfalme wa mwisho wa Babeli kabla ya uvamizi wa Wamedi na Waajemi uliopelekea mwisho wa dola ya Wakaldayo. Kama Daniel alikuwepo enzi hizo aliwezaje kukosea kitu kilicho wazi hivi? Na kama alikosea jambo rahisi kama hili tutaaminije kama kitabu hiki sio utunzi wa Mtu fulani baada ya matukio (ambapo ni rahisi kukosea kwa kuwa hakuwepo)?

Jibu
Danieli ni moja ya vitabu vya Biblia ambavyo vimeshambuliwa sana, na kwa sababu ambayo mtu yeyote aliyeyasoma haya au kuyatafiti atayaelewa. Wenye kushuku na wasioamini Biblia hawana jinsi ya kutimiza malengo yao bila kushambulia vitabu hivi kwa kuwa vimejaa uthibitisho kuwa Biblia haiwezi kuwa Neno la mwanadamu kwa kuwa imetabiri kwa kina matukio, na mambo na falme kwa usahihi kiasi kwamba hakuna namna mwanadamu angeweza kuandika. Moja ya vitabu vya Biblia vyenye unabii huu wa kutisha ni kitabu cha Daniel.

Mashambulizi hayakuanza jana wala juzi. Polfili, mwanafalsafa wa kipagani ni moja kati ya watu wa mwanzo kabisa kukishambulia kitabu hiki. Hatujabakiwa na kazi zake ila tunaweza kujua kupitia wanatheolojia waliokuwa wakijibu mashambulizi haya. Mathalani, Jerome katika maoni yake juu ya kitabu cha Danieli anasema

Polfili aliandika katika kitabu chake cha kumi na mbili dhidi ya unabii wa Danieli, akikana kwamba kiliandikwa na mtu ambaye kitabu hiki kimepewa jina lake, ila mtu mwingine aliyeishi Yudea wakati wa Antiokasi aliyeitwa Epifania. Na zaidi ya hayo anadai kuwa “Danieli” hakutoa unabii juu ya wakati ujao kama ambavyo alisema juu ya wakati uliopita, na mwisho kuwa chochote alichosema mpaka wakati wa Antiokasi kilikuwa ni historia thabiti, wakati chochote alichojaribu kubahatisha zaidi ya wakati ule kilikuwa si kweli, kama ambavyo asingeweza kujua wakati ujao

Mashambulizi ya leo juu ya kitabu hiki aidha ni marudio ya mwanafalsafa huyu, yakiwa yamepakwa rangi ya ukisasa au ni mapya yakifuata msingi wa Polfili. Kitu kimoja ambacho kilimfanya huyu mwanafalsafa afikie hitimisho lake hili ni kuwa maandiko katika Danieli yalitimia hata nukta. Kwa akili timamu ya kawaida kabisa, hakuna namna Danieli angeweza kujua mambo yajayo kwa usahihi hivyo: alijua haukuwa ubahatishaji. Kwa hiyo alibakiwa na njia mbili za kufuata. Aidha Daniel aliandika karne ya 6 K.K au atengeneze namna ya maelezo kuwa ni uhuni uliofanywa baada ya matukio. Bahati mbaya alichagua njia ya pili ambayo siyo ya kweli.

Nikirudi kwenye swali la leo ambalo wengi wa wanaolitumia kama ngao ya kukwepa kuiamini Biblia hufuata nyayo za Polfili, limetokana na kutokuelewa historia na kutojishughulisha. Japo wengi wamelikimbia swali hili na hawalitumii tena, bado wapo wenye kushuku wanaolitumia ili pengine kuwapotosha Wakristo wachanga na wengine wasiojua. Mfano katika maandiko yao, “Skeptic Annotated Bible” wameandika “mfalme wa mwisho wa Babeli alikuwa Nabonidasi aliyetawala toka 556 mpaka 539 and aliyeshindwa na Koreshi. Alikuwa Nabonidasi na si Belshaza aliyekuwa wa mwisho katika wafalme wa Babeli.”

Kwanza hatutumii historia kujaribu kuhukumu Neno la Mungu. Wanahistoria nje ya Biblia wamekuwa wakikosea mambo mengi na hata majina mbalimbali, na unapofanyika ugunduzi wa mambo ya kale, Biblia imekuwa ikithibitishwa kuwa sahihi. Hata hivyo, kwa hili historia ya nje ya Biblia iko sahihi, na Biblia haijakosea. Mfalme wa mwisho wa Babeli hakuwa Belshaza bali Nabodinasi. Na ndio maana Biblia inasema yafuatayo baada ya Danieli kutafsiri maneno yaliyoandikwa na kiganja mbele ya Belshaza:

Ndipo Belshaza akatoa amri, nao wakamvika Danieli mavazi ya rangi ya zambarau, wakatia mkufu wa dhahabu shingoni mwake, wakapiga mbiu kutangaza habari zake, ya kwamba yeye ni mtu wa tatu katika ufalme. (Danieli 5:29)

Hapa Daniel anapaswa kuwa mtu wa tatu kwa kuwa tayari Belshaza alikuwa ni mtu wa pili na kwa hiyo alikuwepo mtu wa kwanza, naam, naye ni mfalme Nabodinasi. Katika andiko la Nabonidus mwenyewe linalofahamika kama "Nyakati za Nabodinasi"[1] tunajua kuwa "Mfalme alitumia miaka kumi huko Araba na akaacha Babeli ikisimamiwa na mwana wake Bel-Shar-Usur [Belshaza]". Kwa hiyo wakati nabonidasi hakuwepo Mfalme wa Babeli alikuwa Belshaza lakini akiwa mtu wa pili na si wa kwanza. Kwa hiyo Biblia hapa ipo sahihi kwa kuwa Danieli, aliyeandika kitabu hiki alishuhudia aliyoyaona.

Kuna Jambo kubwa zaidi ya hili la Danieli kuwa sahihi. Nalo ni kuwa Mungu aliyesema na Danieli, Yeye aliyeumba mbingu na nchi, ametenga siku awahukumu wanadamu wote sawasawa na matendo yao. Mungu atatuhukumu si kwa matendo tu yaliyo maovu bali hata mawazo na nia ovu zote. Siku hii ya kutisha inakuja na njia pekee ya kuepuka hukumu hii ni kujisalimisha kwa Yesu Kristo, yeye aliye mwokozi wa wanadamu wote. Leo hii umlilie yeye, utubu na kugeuka toka njia zako mbaya. Naye atakusamehe makosa yako na kukupa uzima wa milele. Kumbuka Yesu anakuja, furaha kwa watu wake na huzuni, kilio na kusaga meno kwa waliomkataa.

Maranatha!

[1] http://www.britishmuseum.org/explore/highlights/highlight_objects/me/c/cuneiform_fall_of_a_dynasty.aspx

No comments:

Post a Comment